Thursday, 11 September 2014

Athari za utumiaji wa chumvi kupita kiasi


Chumvi inapotumika kwa kiasi kidogo haina madhara. Miili yetu
huhitaji chumvi kwa kiasi kidogo sana. Kwa wastani tunahitaji
chini ya gramu 5 (kijiko cha chai) kwa siku. Hii Huupatia mwili madini ya
sodium yanayohitajika kwa siku. Lakini ni muhimu kukumbuka kwamba mwili
unapata pia madini haya kutoka kwenye vyakula vingine, hivyo chumvi itumike kwa kiasi kidogo. Kwa bahati mbaya tunatumia chumvi kupita kiasi. Matumizi ya chumvi nyingi yanaongeza uwezekano wa kupata shinikizo kubwa la damu,kwani chumvi husababisha maji kujikusanya mwilini. Maji yaliyojikusanya huongeza shinikizo kwenye moyo na mishipa ya damu na hivyo kusababisha moyo kufanya kazi
kwa nguvu zaidi. Shinikizo kubwa la damu huongeza uwezekano wa kupata magonjwa mengine sugu kama yale ya figo, moyo, na pia ya mifupa
kama “osteoporosis”. Hivi karibuni tafiti zimeonyesha uhusiano mkubwa kati ya matumizi ya vyakula vilivyosindikwa au kuhifadhiwa kwa chumvi na saratani ya tumbo. Hivyo ni muhimu kupunguza matumizi ya chumvi.

Jinsi ya kupunguza matumizi ya chumvi
Kupunguza matumizi ya chumvi kutasaidia
kupunguza uwezekano wa kupata baadhi ya magonjwa sugu.
Yafuatayo yatasaidia kufikia lengo hilo:
Punguza chumvi inayowekwa kwenye chakula wakati wa
kupika.
Usiongeze chumvi katika chakula wakati wa kula, pia usiweke chumvi
mezani. Mara nyingi watu huongeza chumvi bila hata kuonja chakula.
Epuka vyakula vilivyosindikwa kwa kutumia au kuongezwa chumvi,
kama nguru aliyekaushwa kwa chumvi, baadhi ya vyakula vya makopo
au paketi, (kama supu za paketi au makopo, “soy souce” michanganyiko
ya kunogesha mchuzi, crisps). Ni vyema kusoma lebo kwa makini na
chagua vyakula vilivyoandikwa “hakuna chumvi iliyoongezwa”(“no salt
added”)
Tumia zaidi vyakula freshi unavyopika mwenyewe kwani unaweza
kuthibiti kiasi cha chumvi unachotumia.
Tumia zaidi viungo kuongeza ladha kwenye chakula, mfano vitunguu
saumu, tangawizi n.k.
Kama umezoea kutumia chumvi nyingi inaweza kuchukua muda kidogo
kujizoesha kula chakula chenye chumvi kidogo au kisicho na chumvi. Jizoeshe
taratibu mpaka uzoee na mwisho utafurahia vyakula vyenye chumvi kidogo au
visivyo na chumvi.

No comments:

Post a Comment

wasiliana nami